Wednesday, October 24, 2012

JK ashauriwa na Kanisa la Kiinjili la Kipentekoste Kufuta Chaguzi Zenye Rushwa

Kanisa la Kiinjili la Kipentekoste Tanzania limemshauri  Mwenyekiti wa Taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete kutoa tamko la kufuta chaguzi zote zizogubikwa na rushwa ndani ya chama hicho ili kurejesha heshima kwa chama na serikali iliyopo madarakani. 

Tamko hilo limetolewa na Mchungaji wa kanisa hilo, William Mwamalanga, katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kufuatia kauli ya Rais Kikwete kwamba vitendo vya rushwa vinavyojitoleza katika chaguzi za CCM vitakitumbukiza chama hicho kwenye shimo. 

Mwamalanga alisema rushwa ndani ya CCM  imekifanya chama hicho kukosa mwelekeo hivyo kinachotakiwa ni kwa Rais Kikwete kuchukua hatua ya kufuta matokeo yote ya viongozi waliochaguliwa kwa rushwa ili kurejesha heshima na imani kwa wananchi kwa chama hicho.

 “Rushwa ndani ya CCM imekuwa zaidi ya malaria, imekuwa zaidi ya ukimwi, kwa msingi huo kauli ya Rais kukemea rushwa haitoshi,maana tatizo hili ndani ya CCM  limebaki kama ngoma isiyokuwa na wachezaji,” alisema Mwamalanga.

Alisema CCM ndiyo chama tawala, hivyo Watanzania walitegema kuona kinakuwa chama cha mfano kupambana na rushwa badala yake kimekuwa kiongozi wa rushwa hali ambayo inazorotesha upatikanaji wa maendeleo nchini. 

Mwamalanga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kurugenzi ya Kueneza Amani kwa Jamii  na dini zote nchini kama tatizo la rushwa litaachwa liendelee kushamiri ndani ya chama hicho kikongwe, itakuwa vigumu kukemea vyama vingine vya siasa iwapo vitachukua madaraka ya nchi. 

Alisema CCM ambayo ilitokana na Tanu ilijiwekea misingi mizuri ya kukataa rushwa, lakini hivi sasa kimekuwa chama kinachoongoza kwa rushwa. 

Kuhusu tatizo la kuchomwa kwa makanisa, alisema serikali inapaswa kuchunguza kwa umakini suala hilo kubaini chanzo na kwamba makanisa yote yaliyochomwa yajengwe kwa gharama za serikali. 

Rais  Kikwete akizungumza wakati wa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT), alitoa onyo kwamba vitendo vya rushwa vinavyojitokeza katika chaguzi za ndani za CCM visipodhibitiwa,  vitakitumbukiza chama hicho kwenye shimo. 

Malalamiko ya rushwa ndani ya chaguzi za CCM yametolewa na baadhi ya wagombea wa uenyekiti wa mikoa. Waliolalamika ni Clement Mabina (Mwanza), John Guninita (Dar es Salaam), Thomas Ngawaiya (Kilimanjaro), Makongoro Nyerere (Mara) na William Kusila (Dodoma).   


No comments:

Post a Comment